Translate in your language

Tuesday, February 7, 2012

Misaada ya China Afrika inavyotesa mataifa ya Ulaya

Misaada ya China Afrika inavyotesa mataifa ya Ulaya

*Yajenga jengo la AU Ethiopia

Na Danny Matiko

UMOJA wa Afrika (UA) hivi karibuni umepata jengo jipya la Makao Makuu yake yaliyopo
mjini Addis Ababa, Ethiopia ambalo limejengwa na China kwa gharama zote.

Jengo hilo la kisasa lenye ghorofa 20, na ambalo ndio refu kuliko yote nchini
Ethiopia, limejengwa kwa vyuma vizito na vioo.

China inasema, jengo hilo ni zawadi yake kwa watu wa Afrika katika kuenzi uhusiano
mwema uliopo kati yake na bara hili.

Jengo hilo lenye urefu wa mita 100 kwenda juu, lina kumbi tatu za mikutano, ukiwemo mkubwa wa kukaa watu 2,500, ofisi zenye uwezo wa kuhudumia watu 700, hadhi
ya kutumiwa na marais wa nchi na mandhari ya kuvutia.

Jengo hilo limejengwa kwenye eneo ambalo kulikuwa na gereza lililotumika kama
kizuizini kwa watu "wote", ambao walikamatwa na utawala wa kijeshi kutokana na kuangushwa kwa Mfalme Haile Selassie wa nchi hiyo mwaka 1974.

Inaelezwa kuwa, wengi wa watu hao waliuawa kikatili wakati wa kampeni iliyojulikana
kama "Red Terror" (ukatili mwekundu), ambayo ililenga kuwaondoa wale wote walionekana kama wapinzani wa mageuzi ya kutoka himaya ya kifalme kwenda mfumo wa Kikomnisti.

Ethiopia ni nchi ambayo haikuwahi kutawaliwa na wakoloni kutokana na imani kwamba, ina mizizi ya ukoo wa Mfalme Sulemani wa Israeli, na hivyo basi wakoloni wa Ulaya
waliiona kama nembo ya Mfalme Daudi wa Israeli ambaye alikuwa Baba yake Mfalme
Sulemani.

Kuna wakati Italia iliivamia kwa lengo la kutaka kuitawala, lakini ilishindikana kwa kuwa majeshi yake yalitimuliwa kwa hasara kubwa kufuatia yale ya Ethiopia kusaidiwa na baadhi ya nchi za Ulaya.

Wakati wa uvamizi huo wa kuanzia mwaka 1936 mpaka 1941, Mfalme Selassie alikimbilia nchini Uingereza ambako alipewa makazi maalumu wakati juhudi za kumrejesha zikifanyika.

Hivyo, hatua ya utawala wa kijeshi kutaka kuibadili nchi hiyo kutoka Ufalme kwenda
kwenye Ukomnisti, zilikumbana na kisiki cha upinzani wa raia na ndipo nguvu kubwa
ikatumika na kupelekea mauaji ya kutisha. Wengi wa waliolengwa ni wasomi, pamoja na
maofisa waliokuwa katika nyanja mbalimbali.

Taasisi za jumuiya kimataifa, ikiwemo ya 'Human Rights Watch', Amnesty
International zimekuwa zikidai kuwa, watu 500,000 waliuawa kikatili, ingawa
Waethiopia wenyewe huamini kuwa idadi hiyo ni ndogo mno, na kueleza kuwa watu
waliouawa ni Milioni moja.

Aliyekuwa kiongozi wa nchi hiyo wakati wa kampeni hiyo ya "Red Terror", Kanali
Mengistu Haile Mariam, ambaye alitawa kuanzia mwaka 1977 mpaka 1987, kwa sasa
anaishi nchini Zimbabwe kama mgeni rasmi wa kitaifa.

Hifadhi hiyo ni fadhila kutokana na kujitolea kwake kuwapatia misaada wapigania
uhuru wa nchi hiyo, wakati wa harakati za ukombozi wa Nchi za Kusini mwa Afrika.

Rasi Robert Mugabe wa Zimbabwe amekuwa akikaririwa akisema "kamwe", Wazimbabwe
hawawezi kumtoa mgeni wao huyo kwa maadui zake.

Kwa upande wa msaada wa China kwa Afrika, zawadi hiyo ya jengo imekuja wakati
mataifa ya Ulaya yanailalamikia kwa kutaka kuhodhi shughuli zote Afrika ikiwemo biashara za kawaida na miradi mbalimbali.

Nchi hizo zinasema kitendo cha China kutoa misaada yake, mikopo nafuu, na zawadi
nyinginezo, bila kuambatanisha na mashariti yoyote kinachangia kwa serikali za Afrika kukiuka haki za binadamu.

Ingawa taifa hilo la Kikomnisti halijawahi jibu madai hayo, yaani "kuchangia
ukiukaji wa haki za binadamu", viongozi wake wamekuwa wakieleza kuwa Afrika ipo
nyuma katika nyanja zote za kimaendeleo na hivyo kuhitaji misaada ya aina mbalimbali ili kujikomboa.

Akifungua jengo hilo la Afrika siku moja kabla ya kuanza kwa kikao cha 18 cha kila
mwaka cha wakuu wa mataifa ya Afrika, Mshauri wa Siasa wa Serikali ya China, Jia
Qinglin anasema zawadi hiyo ya jengo lenye hadhi litabaki kuwa alama ya ushirikiano kati ya Afrika na nchi yake.

Bw. Jia anasema Afrika ndio mshirika mkubwa wa kibiashara wa China, ambapo kwa sasa
mtaji ambao nchi yake imewekeza barani humu ni Dola za Marekani Bilioni 130 (sh.
trilioni 210).

Bila kutaja viwango, kiongozi huyo alifafanua kuwa China itazidisha misaada yake
kwa nchi mbalimbali za Afrika katika kiwango cha kurithisha.

Akipokea jengo hilo jipya, Mwenyekiti wa UA aliyemaliza muda wake, Rais Teodoro
Obiang Nguema wa Guinea ya Ikweta, alisema jengo hilo linaashiria mwanzo mpya wa
Umoja wa Afrika, ambao ulianzishwa Julai 9, 2002, na kuurithi Umoja wa Nchi Huru
za Afrika (OAU) ulioanzishwa Mei 25, 1963.

Jengo hilo lilijengwa kwa miaka mitatu kuanzia 2009, ambapo kulikuwa na jumla ya
wafanyakazi 1,200 wa Ethiopia na China.

Baadhi ya majukumu makuu ya umoja huo ni kuhamasisha umoja na ushirikiano miongoni
mwa Nchi za Afrika ili Bara hili liweze kuwa na sauti moja ya "hapana ua ndiyo"
katika jumuiya ya kimataifa; kuratibu na kukuza ushirikiano miongoni mwa nchi za
Afrika; kulinda uhuru na kutetea hadhi na heshima ya nchi za Afrika na watu wake;
na kutokomeza aina zote za ukoloni popote katika Afrika.

Ingawa inafurahisha na kutia moyo kwamba ukoloni upo ukingoni kutokomezwa, Bara
linatishiwa na aina mpya ukoloni wa kupora rasilimali za nchi, ambapo washirika wa
ukoloni huo ni wananchi wenyewe wa Afrika wenye uroho wa mali na ambao
wanashirikiana na mataifa ya kigeni.

Ni aina mbaya kabisa ya hujuma, kama ilivyowahi kutokea huko nyuma, ambapo baadhi
ya viongozi waliojulikana kama Watemi walishirikiana na wageni kuwapeleka Waafrika
utumwani huko ughaibuni.

Muungano huo pia una taasisi nyingi ambazo zinajishughulisha na masuala mbalimbali
ya kisiasa, kiuchumi, kiulinzi.

Mojawapo ya taasisi hizo ni pamoja na Benki ya Afrika (ADB), yenye makao makuu yake mjini Abdjan nchini Ivory Coast, Afrika ya Magharibi.

Benki hiyo ni mojawapo ya taasisi muhimu za Afrika, zinazodhamini na kufadhili miradi ya maendeleo katika nchi wanachama wa Muungano huo wa Afrika.

Chombo kingine ni Bunge la Afrika ambalo lilianzishwa mwaka 2004. Rais wake wa
kwanza alikuwa Mama Getrude Mongela wa Tanzania, ambaye anasifika kutokana na kazi
nzuri katika kipindi alichotumiakia.

Bunge hilo ambalo wabunge wake huchaguliwa kutoka mabunge ya nchi wanachama wa
Muungano huo, linajumuisha wabunge wa jinsia zote ambao idadi yao ni 265. Makao
yake makuu yapo Midrand nchini Afrika Kusini.

Rais wa sasa ni Idriss Moussa wa Chadi, ambaye alipokea kazi hiyo kutoka kwa Mama
Mongela mwaka 2009.

Mama Mongela ni muhitimu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika taaluma ya Ualimu,
na Dkt. idriss ni mhitimu wa Chuo Kikuu cha Ndjamena, Chadi, katika taaluma ya Udaktari.

Kazi ya Bunge hilo ni kuangalia kama taratibu na utendaji wa kazi za Umoja wa
Afrika zinafuatwa na kutoa ushauri kwa vyombo vya UA.

Chombo kingine cha Umoja wa Afrika ni Taasisi ya kukuza Ushirikiano wa Kibiashara
baina ya Nchi za Afrika (NEPAD) ili kuharakisha maendeleo ya bara hili lote.

Kuna taasisi nyingi za kikanda ambazo zimepewa majukumu yake kulingana makusudio
ya kuanzishwa kwake.

Hata hivyo, ingawa umoja huo umepiga hatua katika kusimamia masuala ya amani katika Afrika, bado kuna changamoto za uhaba wa fedha katika kusimamia mambo ya kiulinzi katika nchi wanachama zenye migogoro.

Mfano ni nchini Somalia, ambapo jeshi la kulinda amani la umoja huo si imara kama
ilivyotarajiwa, ambapo kutokana na udhaifu wa jeshi hilo katika kudhibita upande
unaovunja matakwa ya chombo hicho nchini humo, ni baadhi ya mambao yanayosababisha
amani katika Somalia kuwa kama kitendawili.

Kabla ya kuundwa UA, OAU ndio lilikuwa jina maarufu la umoja wa Bara hili, ambapo watendaji wake wakuu walijulikana kama Makatibu Wakuu wa OAU.

Wengi wa viongozi hao ambao walikuwa wanadiplomasia mahiri, walifanya kazi nzuri
ya kuratibu ushirikiano baina ya nchi zote za Afrika na kuiweka Afrika katika
hadhi yake.

Hao ni Katibu Mkuu muasisi, Bw Kifle Wodaji wa Ethiopia aliyetumikia kuanzia mwaka
1963 mpaka 1964.

  Wengine ni Diallo Telli wa Guinea-Konakry (1964-72); Nzo Ekangaki (1972-74) na
William Eteki (1974-78), wote wa Kameruni.

Edem Kodjo, Togo (1978-83); Peter Onu, Nigeria (1983-85); Ide Oumarou, Niger
(1985-89); Salim Ahmed Salim, Tanzania (1989-2001); na Amara Essy, Ivory Coast
(2001-2002).

  Dkt. Salim ndiye anashikilia rekodi ya kuutumikia Umoja huo kwa muda mrefu wa miaka
12 mfululizo, na pia ndiye alisimamia maandalizi ya kuanzishwa UA.

Miongoni wa viongozi wa Afrika waliosimama kidete kuhakikisha umoja huo wa OAU
unabaki kuwa imara, ni pamoja na Mwalimu Julius Nyerere ambaye pia mwaka 1984
alikuwa Mwenyekiti wake.

Rais Jakaya Kikwete alikuwa Mwenyekiti wa UA mwaka 2008 mpaka 2009.

Katika mkutano wa 18 wa viongozi wakuu hao wa Afrika uliofanyika mjini Addis
Ababa wiki iliyopita, ulishindwa kumchagua Kamishina Mkuu wa Umoja huo, baada ya
aliyekuwepo, Jean Ping wa Gabon, kutaka kuchaguliwa tena kuendelea katika nafasi
hiyo.

Mvutano ulikuwa kati ya Dkt Ping (69), ambaye ni raia wa Gaboni mwenye asili ya
China, na Bi Nkosazana Dlamini-Zuma (63), ambaye ni mke wa zamani wa Rais Zuma wa
Afrika ya Kusini.

Katika upigaji kura za siri, viongozi hao hawakumchagua yeyote kati ya wawili hao,
ambao kutokana na kanuni za UA, wote sasa wamepoteza nafasi ya kuwania tena
kuchaguliwa.

Umoja huo sasa unaongozwa kwa muda na Bw Erastus Mwecha wa Kenya mpaka mwakani
2013 atakapochaguliwa Kamishina mpya katika mkutano wa 19 wa wakuu hao
utakaofanyika nchini Malawi.

Bw. Ping, ambaye alisomea uchumi katika Chuo Kikuu cha Paris, nchini Ufaransa, baba
yake ni mfanyabiashara wa China  liyehamia Gaboni miaka ya 1930 na kumuoa Mgaboni.

  Mwaka jana 2011 alilalamikiwa sana na baadhi ya nchi za Afrika kwa kushindwa
kuchukuwa hatua za haraka na zilizofaa dhidi ya uvamizi wa Mataifa ya Magharibi
kule Libya, ambapo kiongozi wa nchi niyo Kanali Muammer Gaddafi aliuawa.

  Kanali Gaddafi alikuwa mfadhili mkuu wa UA katika masuala mbalimbali ya dharula,
yaliyohitaji kujitolea katika kuchangia fedha za baadhi ya mahitaji ya Umoja huo.

No comments :

Post a Comment

here u,re comments/acha ujumbe wako hapa

Kijiweni (nipe 5)