Translate in your language

Wednesday, March 15, 2017

Dk. Kigwangalla aongoza ujumbe wa Tanzania kwenye mkutano wa CSW 61



Dk. Kigwangalla aongoza ujumbe wa Tanzania kwenye mkutano wa 61 wa Kimataifa wa Kamisheni ya hali ya Wanawake Duniani

NEW YORK: Naibu Waziri wa Afya , Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mheshimiwa Dkt. Hamisi Kigwangalla (Mb)  ameongoza ujumbe wa  Tanzania wa wizara zinazohusika na mambo ya uwezeshaji wa wanawake kiuchumi za Tanzania Bara na Zanzibar  juu ya uwezeshaji wa Wanawake Waliopo kwenye sekta isiyo rasmi, mjini New York City, Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, kwenye Mkutano wa 61 wa Kimataifa wa Kamisheni ya Hali ya Wanawake Duniani. 
Katika hotuba yake katika mkutano huo wa Mawaziri wa Wanawake Duniani, Dk. Kigwangalla ameeleza mambo mbalimbali ikiwemo hatua tulizofikia kama nchi kwenye kuleta usawa wa kijinsia na ukombozi wa mwanamke wa kitanzania hususani kiuchumi ikiwemo vikwazo vya kimila vinavyomfanya mwanamke kuwa wa hali ya chini kwenye jamii, pamoja na changamoto anazokumbana nazo mwanamke kwenye ajira zisizo rasmi (informal sector) ambapo wanawake ni wengi (asilimia 82) ukilinganisha na wanaume (asilimia 72).
"Ilikufikia malengo, Jitihada za serikali za nchi yetu kuanzia kuweka usawa wa kijinsia na kupinga ubaguzi kuanzia kwenye katiba yeti, sera ya mikopo midogo midogo, sheria zinavyoweka sharti la mali za wanandoa kutowekwa dhamana ama kuuzwa kama mwanandoa mmoja hajaridhia, uanzishwaji wa mfuko wa maendeleo ya wanawake kwenye halmashauri zote 114 Tanzania bara ambapo asilimia 5 ya bajeti ya mapato ya ndani ya halmashauri ni lazima iende kwa wanawake.
Pia jitihada tunazofanya kuwahamasisha wanawake wamiliki mali, warasimishe biashara zao (Mkurabita), pia waraimishe vikundi vyao vya kuweka akiba na kukopa na vya kusaidiana" Ameeleza Dk. Kigwangalla kwenye mkutano huo.
Aidha, Dk. Kigwangalla amebainisha kuwa, kwa upande wa Tanzania, Serikali imepiga jitihada kubwa kuhakikisha inamkomboa mwanamke kutoka kwenye utegemezi kwa kuunda vyombo mbalimbali na kuandaa sera na miongozo inayoelekeza usawa katika kufikia malengo ya kumkomboa mwanamke kiuchumi ambapo mwanamke anakuwa na haki na uwezo wa kukopa katika taasisi mbalimbali ili kuanzisha au kukuza mtaji wa biashara yake katika kufikia malengo aliyotarajia.
Vile vile imeanzisha mfuko wa maendeleo katika halmashauri zote 114 nchini ili kuwafikia wanawake walio wengi zaidi, imeendelea kuhamasisha Jamii kuanzisha  mifuko mbalimbali ya kuweka na kukopa kama vile (VIKOBA) , kuwahamasisha kushiriki katika maonyesho mbalimbali ya kitaifa na hata mikutano mikubwa ya kimataifa ili kujitangaza na kukuza bidhaa mbalimbali kwa lengo la kujipatia kipato na kukuza mitaji yao.

Ameongeza k uwa, kufanya hivyo, kunawasaidia kutengeneza mitandao ya kibiashara itakayowasaidia kukua kimataifa na kufanya biashara Kubwa za kimataifa na pia kutoa ajira kwa Wanawake wenzao . Pia Serikali imeanzisha benki ya Wanawake ambayo Kazi yake Kubwa ni kutoa mikopo na ushauri ambao utawasaidia  kukuza biashara zao na kuongeza kipato kwani Wanawake ni Jeshi kubwa ambalo linachangia uchumi wa nchi kwa kiasi kikubwa.

No comments :

Post a Comment

here u,re comments/acha ujumbe wako hapa

Kijiweni (nipe 5)