Translate in your language

Sunday, December 19, 2010

FAIDA NA HASARA ZA MFUMO WA CLOUD

Miaka michache iliyopita  watu wengi waliokuwa wanatumia teknohama kwenye shuguli zao za kila siku walikuwa na tatizo sugu la kuhifadhi taarifa na nyaraka zao mbalimbali wanazofanyia kazi wakati huo watu wengi walikuwa wananunua vifaa vyenye nafasi kubwa kwa ajili ya kuhifadhi taarifa hizo na mengineyo .

Ushahidi uliowazi ni jinsi kampuni Fulani ilivyokuwa  inahaha kuongeza ukubwa wa HDD na kila mfanyakazi kwenye kampuni hiyo kununuliwa flashdisk yake au chombo chake cha kuhifadhia mali zake ili aweze kuwa nazo popote anapoenda kwenye shuguli mbalimbali .

Lakini kukawa na tatizo lingine pia kwamba mfanyakazi anaweza kuwa yuko mtwara na komputa yake ikaharibika au hicho kifaa cha kuhifadhia taarifa zake kikaharibika au kuibiwa au hata vyote kifaa hicho , komputa na mengine yote yakaibiwa au kuharibika tu kampuni inakuwa imepata pigo la kiutendaji .

Huo ni mfano mdogo wa jinsi watu na kampuni zilivyokuwa na hofu sana na taarifa zao wakati huo .

Hofu hii kwa sasa imepungua kwa kiasi kikubwa au kama sio kuisha kabisa lakini ujio wa tovuti kama wikileaks pia umeleta hofu kwa teknologia zingine za kuhifadhi taarifa au kushirikiana taarifa na wengine wanaofanya kazi kwa vikundi .

Kuja kwa mifumo mbalimbali ya mawasiliano kwa njia ya Mtandao Maarufu kama CLOUD kumebadilisha kwa kiasi kikubwa hofu na mashaka mengi ambayo watu wengi waliokuwa nayo wakati huo ambapo kila mtu alipenda kununua kifaa chake kwa ajili ya kuhifadhia taarifa .

Hofu ya hufadhi na kutumia taarifa imepungua kwa kiasi kikubwa sana kwa sababu kwenye mfumo wa CLOUD unaweza kuhifadhi taarifa na mambo yako mengine kwa njia ya mtandao na kuweza kuchukuwa taarifa hizo ukiwa sehemu nyingine yoyote duniani yenye huduma ya mtandao na hata unaweza kumpa ruhusa mwingine aliyopo popote duniani kuangalia au kufanyia kazi taarifa hizo kutoka popote duniani .

Kampuni kubwa ya masuala ya teknohama duniani iliyowekeza kwenye mfumo wa CLOUD kwa kiasi kikubwa ni IBM mbayo ina Vituo vya kuhifadhia Taarifa ( DATA CENTRES ) sehemu kadhaa duniani na inatoa huduma za kuhifadhi taarifa kwa kampuni nyingine kubwa kama mabenki , mashirika ya umma na taasisi zingine za umoja wa kimataifa .

Kampuni lingine ni GOOGLE ambalo lina programu nyingi zinazotumika kwenye mfumo huu kama GOOGLE DOCS , Microsoft Nao wana programu kadhaa ambazo ziko kwenye mfumo huu .

Kwa kutumia programu hizo kuna watu sasa hivi wanaweza kufungulia barua pepe za maofusini kwao toka popote duniani kujibu na kufanya shuguli zingine kwa ruhusa tu .

FAIDA ZA CLOUD.
1 – Faida yake kuu ni kwamba kampuni ni ndogo na kubwa zinazotumia teknohama zinaweza kutumia aina moja ya program na vitu vingine kwa faida bila ya kuwa na miundombinu ya ziada kama ikiwepo basi ni ya gharama ndogo sana .

2 – Mtu mmoja anaweza kutembelea Sehemu za kuhifadhia taarifa ( DATA CENTRES ) nyingi kwa wakati mmoja duniani kwa mguso mchache wa Kipanya chache cha komputa na kutokea popote .

3 – Pia kampuni au watu wanaweza kuongeza vitu na mengine mengi bila ya kulipiga gharama za ziada lakini hii inategemeana na aina ya huduma ambayo inatolewa kwa wakati Fulani .

4 – Mfumo huu uko salama na masuala ya uchafuzi wa mazingira kwa sababu si vitu vingi vinatumika lakini hakujawa na utafiti zaidi wa adhari zake za kiafya kwa watumiaji wa huduma hizi .

Kwa siku za mbeleni mfumo wa CLOUD utakuruhusu kununua komputa ndogo , bei nafuu na monitor yako , hautohitaji vitu kama CDROM Au Hard Disk Lakini utatakiwa kuwa Umeunganishwa na mtandao tu kuweza kufanya shuguli zako za kila siku .

Pamoja na mazuri hayo niliyoyataja hapo juu pia kuna athari zake kwa baadhi ya vitu endapo mfumo huu utafanikiwa kupenya na kutumika kwa wingi zaidi duniani .

ATHARI ZA CLOUD
1 – Kunaweza Kuwa na ongezeko la Gharama za kusafirisha Taarifa kwa njia ya mtandao kutokana na ukubwa wa taarifa hizo .

2 – Kwenye mfumo huu ni kampuni zingine ndio zinahifadhi taarifa zako yaani zinazotoa huduma za kuhifadhi taarifa zako kwahiyo hautokuwa na uwezo wa kutembelea komputa hizo au program zake kinachokuhusu wewe ni taarifa zako tu .

3 –  Inaweza kuwa vigumu kuhamisha taarifa nyingi na kubwa kwa wakati mmoja endapo tatizo limetokea sehemu Fulani labda Mtandao ukiwa taratibu na matatizo mengine mengi .

4 – Taarifa zinazohifadhiwa zinaweza kuwa si salama sana na zinaweza kupotea kwa njia nyingine au kutembelewa na wahalifu popote walipo duniani tofauti na vile unavyohifadhi kwenye flashdisk yako .

5 – Programu zinazotumika kwenye mfumo wa CLOUD hazina vitu vingi kama zilivyo programu zingine za kufanyia kazi zinazoingizwa kwenye komputa za kawaida .

CHANGAMOTO MPYA ZA CLOUD
Sheria za mitandao ( cyberlaw ) za nchi nyingi haziendI sambasamba na mfumo wa CLOUD lakini wananchi wake na mashirika yake labda yanatumia mfumo huu kuna haja sasa ya kwa nchi nyingi kutambua rasmi mfumo huu na kuweza kutengeneza sheria za mitandao zinazoendana na mfumo huu .

Suala la mwisho ni leseni kwa program zinazotumika kwenye mfumo huu , mfano zamani hata sasa hivi unaweza kuuziwa leseni kwa ajili ya komputa moja au kumi na leseni hiyo ikawa ni kwa ajili ya nchi za asia tu lakini ukija kwenye mfumo huu leseni ya program inaweza kutumika na mtu popote duniani na ndio shida inaanzia hapo .

Hayo ni mambo machache kuhusu mfumo wa CLOUD naamini serikali yetu imeshaona hii pamoja na wataalamu kadhaa ma masuala ya teknohama kusoma na kufanyia utafiti tuone nchi yetu inaweza kufaidika vipi na mfumo huu kwa siku zijazo kutokana na gharama zake .

Jambo la msingi la kuzingatia ni kwamba faida zake na athari zinaweza kutofautiana kutegemeana na kampuni zinazotoa huduma hizo na sehemu ambayo mtu Fulani yupo .

YONA FARES MARO
Sunday, December 19, 2010

1 comment :

Anonymous said...

ahsante kwa taarifa zilizo za faida na nzuri

Post a Comment

here u,re comments/acha ujumbe wako hapa

Kijiweni (nipe 5)